OTHER WEBSITE LISTS


Thursday, December 29, 2011

Mauti si ya Kafulila ni mabaki ya ‘zidumu fikra za Mwl

WIKI iliyopita Mbunge wa Kigoma Kusini, (NCCR Mageuzi) Bw. David Kafulila, aligeuzwa ndama wa kafara ili kuhitimisha mgogoro uliokikumba chama chake, alipovuliwa uanachama na kikao cha dharura cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama hicho, hiyo inamaanisha kuwa kijana huyu mwenye umri wa miaka 29 tu, amepoteza ubunge wake, labda utokee muujiza.

Ni bahati mbaya kuwa mwisho wa Kafulila umekuwa hivyo, na haukuwa kama rafiki yake wa siku nyingi Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA), ambaye aliweza kuruka vihunzi akafanikiwa kubaki chamani, japo mpango ulisukwa kumtoa. Naam si hao tu, Mbuge wa Jimbo la Wawi kupitia (CUF) Hamad Rashid, naye amekalia kamba ya katani mlimani wakati wowote inaweza kukatika, tayari hoja ya kumfukuza uanachama imewasilishwa chamani na vikao vinaandaliwa. Kisa katofautiana na viongozi wenzake.

Matukio haya matatu, pamoja na yale yanayoendelea ndani ya CCM, yanaashiria jambo moja kubwa! Tatizo la kimfumo na mabaki ya dhana ya iliyotamalaki katika awamu ya kwanza ya utawala wa Tanzania iliyosema; ‘zidumu fikra za Mwalimu,’ ambayo haikutoa nafasi kwa watu ndani ya chama kutofautiana kwa hoja na bado kuendelea kubaki pamoja.

Tukio hilo ambalo kabla ya kufikia uamuzi wake, kulikuwa na misuguano mingi ndani ya chama cha NCCR Mageuzi, huku kukiwa na pande mbili za wanaomuunga mkono Kafulila na wale wa upande wa Mwenyekiti wa Chama hicho, Bw. James Mbatia, ambapo kwa ujumla wake ilionekana kwamba, Kafulila alikuwa akikinzana na iongozi wa chama hicho kimtazamo.

Itakumbukwa kuwa, mfumo wa siasa za vyama vingi ulianza mwaka 1985, ukirithi ule wa chama kimoja, ni mchanga na wala haujawa na mizizi mizito ndani ya viongozi, vyama na wananchi kwa ujumla. Dhana ya ujamaa ambayo hasa ilijenga msingi wa ‘zidumu fikra za Mwalimu’ umesalia hata kwenye katiba, japo kinachofanyika ni uchumi wa soko.

Pia katika siasa za nchi, mfumo unabaki ule ule wa ‘Zidumu fikra za Mwalimu, yaani mtu mmoja afikiri na wengine watekeleze, hakuna kuhoji wala kujadili mawazo mengine, badala yake utaitwa muasi na kikao kitaitwa kukushushia rungu kichwani.

Ninachotaka kujadili hapa ni ukweli uliofichwa nyuma ya pazia kuwa wabunge, wanachama na hata viongozi wa ngazi za chini katika vyama vyetu vya kisiasa hawako huru kifikra wanapaswa kudumisha fikra za wenyeviti wao na wapambe wao.

Simaanishi kuwa, hawa wahusika mmoja mmoja ambao wamefikishwa kwenye mabaraza ya juu wakitishiwa kuvuliwa uanachama hawana hatia, laa hasha! lakini ninalotaka kuonesha hapa ni kuwa kuna jambo la zaidi ya makosa au uasi wao.

Ninalotaka lionekane hapa ni ukweli mwingine kuwa, ndani ya vichwa vya akina Mbatia, Mbowe, Profesa Lipumba na hata Jakaya Mrisho Kikwete, kuna mabaki ya dhana ya ‘zidumu fikra za Mwalimu’ ambayo yanawanyima nafasi ya kutambua kuwa, wanaweza kutofautiana katika falsafa, lakini wakandelea kufanyakazi pamoja.

Kilichotokea kwa Kafulila, kiliwahi kutokea Zambia, ambapo rais aliyekuwa madarakani alitofautiana na wenzake chamani, lakini kwa kuwa mfumo wao wa sheria ulikuwa umeshaondolewa kwenye dhana ya zidumu fikra ukamuokoa, akaanzisha chama chake haraka na akaendelea kutawala akiwa na chama kipya.

Mchungaji Christopher Mtikila, aliliona hili mapema, akaamua kufungua kesi mahakamani akipinga dhana ya kikatiba ya kuzuia mgombea binafsi, akashinda kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, lakini jopo la majaji, lililoongozwa na aliyekuwa Jaji Mkuu Augustine Ramadhani, aliamua kuwa Mahakama haina mamlaka ya kikatiba ya kuiamuru serikali kuondoa kifungu cha katiba kinachozuia mgombea binafsi na wakati huo, kulikuwa na siku chache tu kabla ya uchaguzi mkuu kuitishwa.

Ni hukumu hii tata ambayo ilidai eti suala hilo ni la kisiasa, hivyo linastahili kujadiliwa katika majukwaa ya kisiasa iliyoendeleza dhana hii chafu hadi leo, ambayo kwa hakika ni mauti mazito katika siasa za Tanzania.

Ninaamini moyoni mwangu kuwa, ni mauti hii ya demokrasia inayokuza ufisadi kuanzia ndani ya vyama hadi serikalini kwa kuwa watu wamewekwa kufuli mzito midomoni wakithubutu kupinga jambo lolote, wanaitwa waasisi wanafukuzwa na wale wenye mamalaka wanalindwa na mfumo uliopo .

Lakini kama Jaji Ramadhani, katika hukumu yake angezingatia ukweli mwingine kuwa Mahakama ndicho chombo chenye mamalaka ya kisheria, kutafsiri sheria na kutoa haki iliyominywa, angeruhusu mgombea binafsi kwa kuwa hiyo ndiyo hukumu ya haki.

Kwamba kuna mgogoro wa kikatiba na kifungu cha kisheria kimewekwa kwa madhumuni ya kuminya haki za wengine, na kinakiuka haki za kibinadamu na shauri lipo mbele ya Mahakama, ni chombo hicho chenye haki ya kutafsiri na kutoa hukumu na wala si kingine.

Kwa maoni yangu, Jaji Augustine Ramadhani, hawezi kusahaulika kutokana na hukumu hii na nadhani iko siku ataungana nami kujutia maamuzi yake, ambayo leo yanamsindikiza Kafulila mitaani na kuliacha jengo la bunge Dodoma, kubaki katika historia tu huku ikikiacha chama cha NCCR Mageuzi, kubakia na wabunge watatu tu.

Sio Kafulila ambaye amekutana na maswahiba ya namna hiyo, madiwani watano wa CHADEMA, wakitokea Arusha nao walishindwa kufurukuta baada ya maamuzi ya chama hicho, kuwavua uanachama na kuwafanya wapoteze ridhaa ya wananchi ya kuwachagua kuwa, madiwani wao kwenye maeneo yao mkoani humo.

Watu wengine ndani ya NCCR- Mageuzi, ambao waliambatana na Kafulila ni pamoja na aliyekuwa mgombea wa chama hicho, kwa nafasi ya urais 2010, Hashimu Rungwe, ukiachilia mbali wengine 16 waliopewa onyo kali.

Tanzania kwa ujumla tunapaswa kutambua kwamba, kiongozi si mtu anayejua yote, kuna wakati anaweza kukosea na tujifunze kukubali makosa, pale tunapokuwa tumekosea na si kung’ang’ania eti kwa kuwa ni kiongozi.

Ufisadi mkubwa ambao leo tunaweza kuuona kwenye maeneo mbalimbali ni kutokana na watu kuogopa kusema ukweli, mtu anaogopa kwa kile anachohisi kwamba watu wengine watamuona muasi, tena mwenye kimbelembele. Ni wakati ambao tunatakiwa kubadilika kutoka kwenye fikra za; nitaonekanaje na tujijenge kwenye ukweli na uwazi pale penye ukweli.

Vyama vingi vya siasa Tanzania tumejaribu demokrasi, tunaona tutaweza na hata kusonga mbele, ikiwa tu tutaachana na siasa za woga na kusimamia haki hatakama itatugharimu kwa muda. Ni wazi kuwa huu ni wakati wa kujenga upya siasa zetu tukiwa tayari kulipa gharama ya demokrasia kama ile watangulizi wetu waliyolipa. Ninapowaaga nawashauri watanzania wote kujitambua kuwa wao ndio wajenzi wa siasa safi na utamaduni wa ukweli na uwazi, wanapaswa kusema ndio wakamaanisha ndio na hapana wakamaanisha hapana, wasimpigie makofi fisadi wakimtazama usoni, lakini akiwapa kisogo wanamsonda vidole.

Niweke kalamu yangu chini nikisisitiza kuwa maadui wa Tanzania ya leo ni Watanzania wenzao, ambao wamebobea kwenye unafiki na uzandiki wa kutisha ambao wakiibiwa wanacheka, wakidhulumiwa wanacheka na wakidanganywa wanashangilia usoni japo mioyoni wanalia!

Tuesday, December 27, 2011

IS CHRISTMAS A DAY OR JUST A MESSAGE?



KRISMAS NI SIKU AU NI UJUMBE?

Napenda nianze kwa kuomba radhi msomaji wangu kwa kukatisha makala ya “Masuala yaliyopo leo katika tafsiri za unabii” ambapo sasa tunatazama swali: “Je, kanisa litapita kwenye dhiki kuu? “Makala hiyo tutaendelea nayo wiki ijayo, ila nimewiwa moyoni mwangu leo kukushirikisha ujumbe maalum wa Krismas leo ikiwa ndiyo siku yenyewe. Katika ujumbe huu tutajadili mada niliyoipa jina KRISMAS NI SIKU AU NI UJUMBE?

Katika sikukuu zinazosherehekewa kwa msisimko mkubwa duniani, hakuna inayofikia Krismas. Utafiti unadhihirisha kuwa sikukuu hii inasherehekewa kwenye mataifa mengi duniani kama sikukuu ya kidini na pia ya kitaifa (public holiday). Hii hufanywa hata na baadhi ya mataifa yasiyofuata mwelekeo wowote wa dini. Mambo yafanyikayo katika sikukuu hii mfano, kupambwa kwa mti wa Krismas, kubadilishana zawadi, kutembeleana n.k, yana mizizi yake tokea mbali sana kihistoria. Dunia imekuwa ikisherehekea siku hii kama kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa kwa Bwana Yesu Kristo.

Lakini ni wachache sana duniani wanaofahamu kuwa kwa kweli Yesu hakuzaliwa tarehe 25 Desemba, wala kwamba tarehe hiyo haina uhusiano wowote na ujio wake duniani. Labda la kushtua zaidi ni ule ukweli kuwa siku hii ilianza kusherehekewa kwa mara ya kwanza mwaka 350 BK (wengine husema ni 354 BK) kama siku ya kuzaliwa kwa Yesu ikiwa na lengo la kubadilisha sikukuu ya kipagani ya Saturnalia iliyokuwa ikiheshimiwa sana siku za dola ya Rumi, kuwa ya Kikristo. Pengine utaniuliza, “kama ni hivyo, je, mchungaji huoni kuwa ni makosa kabisa kusherehekea Krismas kwa kuwa ni kama kuabudu miungu ya uongo, tena ni kudanganya kuwa ni ‘birth day’ ya Yesu wakati sivyo?” Hili ndilo swali na hoja ya wengi wasioamini kuwa ni sahihi kuadhimisha Krismas, na ndiyo maana natamani tujadili leo, ili tuone maana ya kweli ya Krismas na umuhimu wake kwa waamini wa kweli leo. Neno kuu tutakalojifunza hapa ni ule ukweli kuwa Krismas sio siku, ila ni ujumbe tuupatao kutokana na lile tukio la kuja kwa Mwokozi duniani.

Kama mtu akiitazama Krismas kama siku na akaadhimisha siku hiyo kama “birth day” ya Yesu, kama ni mtafiti wa mambo atagundua haraka sana kuwa amekuwa akiadhimisha siku ambayo siyo yenyewe. Lakini baya zaidi, atakuwa amekosa ile maana yenyewe ya tukio la ujio wa Yesu duniani, na hivyo kuadhimisha kwake kutakosa maana. Kwa sababu hii vyema tujifunze undani wa Krismas ili tunaposherehekea tusiwe kama wachezao ngoma wasioijua. Kwa kuanza hebu tuangalie kwa ufupi maana ya neno “Krismas” na historia yake.

Neno “Krismas” wala tarehe ya kuzaliwa kwa Bwana Yesu havipo kwenye Biblia. Hatuna budi kurejea historia ya Ukristo tuone asili ya neno na historia yake. Huku kutokuwapo mambo haya kwenye Biblia kwenyewe kunaonesha dhahiri kuwa Roho wa Bwana hakuona umuhimu wa kutilia uzito kwenye siku au tarehe ya kuzaliwa kwa Yesu, ila alitilia uzito kwenye tukio na ujumbe wa tukio lenyewe, kama walivyoandika Mathayo na Luka. Kama tutakavyoona, hata kanisa la kwanza halikutilia mkazo kwenye tarehe au siku ya kuzaliwa kwake, ila maana na uzito wa ujio wake. Hebu tuone ituambiavyo historia kuhusu Krismas:

Maana ya Neno Krismas na Historia yake

Neno "Krismas" kama linatokana na neno la kiingereza "Christmas" ambalo likitafsiriwa moja kwa moja (transliteration) linakuwa "Christ's Mass" ikimaanisha "Kusanyiko la Kristo." Kwa mujibu wa encyclopedia ya Wikipedia, tarehe au mwaka wa kuzaliwa kwa Yesu hasa haujulikani, ila inakisiwa ni kati ya mwaka 7-2 BK. Kabla ya mwaka 350 BK siku ya kuzaliwa kwa Yesu iliadhimishwa tarehe 6 January. Mwaka huo (350) kwa uamuzi wa kanisa la Rumi tarehe 25 Desemba ilianza kutumiwa kama sikukuu ya kuzaliwa kwa Yesu. Hii ni kwa mujibu wa kitabu cha Earle E. Cairns kiitwacho Christianity Through the Centuries (1954, 120).

Kabla ya hapo tarehe hiyo ilitumiwa na wapagani wa Rumi kuabudu mungu wao aliyeitwa Saturn. Katika ibada ya Saturnalia watu walipamba miti, na kupelekeana zawadi. Wengine walitembea uchi mitaani, vitendo vya uasherati na kuua, vilikuwa sehemu ya ibada hiyo. Wapagani hao walipotakiwa kuacha upagani na kuukubali ukristo waliona kuwa kikwazo ni kuacha kuadhimisha siku ya Saturnalia. Kanisa la Rumi likawaruhusu waabudu siku hiyo lakini sio kama kwa mungu Saturn, bali kama kuadhimisha kuzaliwa kwa Bwana Yesu Kristo. Hii inashuhudiwa na wanahistoria wengi sio Cairns pekee. Leo ukifanya utafiti kidogo tu kwenye google utakutana na hilo kwa wingi sana.

Kilichofanywa na kanisa la Rumi, yaani kuwaingiza wapagani kanisani kwa kutengenezea sikukuu inayoendana na siku yao ya kipagani kuliifanya hatimaye ibada yao ya kipagani ife kabisa. Lakini kwa kweli hakukuwabadilisha mioyo yao wala hawakugeuka kuwa Wakristo wa kweli. Walipokea dini kama dini lakini sio uzao mpya mioyoni mwao. Historia inatuambia kuwa wapagani hao walikuwa wanasherehekea sikukuu ya kuzaliwa kwa Yesu Kanisani, lakini wakitoka kanisani vile vitendo vya kipagani waliendelea navyo kama kawaida. Hii ni kusema kuwa siku pekee haitoshi kumbadilisha mtu, wala kuadhimisha siku hakumuokoi mtu yeyote.

Tuseme nini basi kwa habari ya siku ya terehe 25 Desemba kuwa Krismas, yaani kusanyiko la Kristo linaloadhimisha kuzaliwa kwa Mwokozi Yesu? Je, kwa kuwa mwanzo wake kihistoria ni dhaifu kiasi hicho ni dhambi kuadhimisha kuzaliwa kwa Yesu. Je, tunapoadhimisha Krismas tarehe hii ya leo huku tukijua kuwa kweli Yesu hakuzaliwa tarehe kama hii ya leo tunamkosea Mungu wetu? Je, tufanyapo haya tunajiunga na wale wapagani kuabudu mungu Saturn kama wengine wasemavyo? Je, tuache kabisa kutambua kuzaliwa kwa Yesu.

Jibu la hayo yote lipo kwenye kutofautisha kati ya kuiadhimisha siku kama siku, na kuadhimisha tukio la kuzaliwa kwa Mwokozi Yesu. Kama tukitukuza siku ya tarehe 25 Desemba, kana kwamba ni siku takatifu ya kuzaliwa kwa Yesu, na kuadhimisha kwetu tukakujenga kwenye siku kama vile ni "birthday ya Yesu" tutakuwa tunakosea. Kwanza kwa sababu uzito wa kuja kwa Yesu haupo kwenye siku au tarehe ya kuja kwake bali kwenye maana na ule ujumbe utokanao na kuja kwake. Pili kwa sababu siku au tarehe haituongezei wala kutupunguzia kitu chochote kiroho hata tuitukuze na kuiadhimisha. Kama ingekuwa muhimu kiasi hicho basi Biblia ingetuwekea mazingira ya kujua tarehe ya kuzaliwa kwake na kutuagiza tuiadhimishe, lakini iko kimya kwa habari hiyo. Tatu sio sahihi kusema kuwa Yesu alizaliwa tarehe ambayo hakuzaliwa.

Lakini kama tukiiona tarehe 25 Desemba kama siku tuliyoitenga kutafakari tukio la kuja kwa Yesu Kristo duniani, siyo kwa sababu ndiyo tarehe aliyozaliwa, wala siyo kwa lengo la kuwafanya wapagani waukubali Ukristo kama lilivyofanya kanisa la Rumi, bali kwa sababu kuzaliwa kwa Yesu kuna umuhimu na uzito unaostahili na unaokubalika kibiblia kusherehekewa na kuzingatiwa na wafuasi wa kweli wa Kristo tunatenda vyema, naam, vyema sana.

Neno kubwa hapa ni ule mtazamo tunaokuwa nao kuhusu ile siku, kunakotokana na mahali , yaani hatua tulipo kiroho. Mara nyingi watu walio wachanga kiroho wanapofahamu kuwa kumbe tarehe ya kuzaliwa kwa Yesu siyo hii, na ya kwamba mazingira yaliyopelekea hata tarehe hiyo itumike kuadhimisha kuzaliwa kwa Yesu ndiyo hayo, dhamiri zao changa hutishiwa usalama, wakidhani kuwa wakiadhimishisha Krismas watakuwa wanaabudu miungu au watakuwa wanasema uongo. Lakini tukumbuke kuwa hakuna siku ya shetani, bali siku zote ni za Bwana. Kwamba kuna watu waliowahi kuabudu miungu siku au tarehe fulani kihistoria, hakutuzuii leo kumwabudu Mungu wetu siku au tarehe hiyo. Tusifanye makosa ya kumkabidhi shetani siku.

Kama kanisa la Rumi lingewapa Injili ya kweli wale wapagani, wakaokoka, kisha wakawaambia kuwa badala ya kufuata ibada mfu za Saturnalia, afadhali siku hiyo mtafakari wema wa Mungu wetu aliyetupenda hata akatuletea zawadi ya Mwanawe wa pekee atuokoe, wangefanya vyema. tatizo halikuwa kwenye kubadilisha siku kutoka kuwa siku ya kumwabudu shetani kuwa siku ya kumwabudu Bwana. Tatizo lilikuwa kuwapa wapagani siku kidini badala ya Yesu mwenyewe aokoaye.

Ujumbe wa Krismas ni Neema ya Mungu sio Siku

Ni sahihi kusherehekea Krismas, tena inapasa, kwa nini? Kwa sababu kwanza, mbingu zinatupa mwongozo huo. Alipozaliwa Yesu Mungu alifanya "Krismas" ya kwanza kwa kupeleka Malaika kondeni walikokuwa wakichunga kondoo wachungaji. Unakumbuka ujumbe wa Malaika hao? Hebu tukumbushane walivyosema:

Malaika akawaambia, "Msiogope, kwa kuwa mimi nawaletea HABARI NJEMA YA FURAHA KUU ITAKAYOKUWA KWA WATU WOTE, maana leo katika mji wa Daudi amezaliwa KWA AJILI YENU Mwokozi ndiye Kristo Bwana"....Mara walikuwapo pamoja huyo Malaika, wingi wa jeshi la Mbinguni wakimsifu Mungu na kusema; Atukuzwe Mungu juu mbinguni, na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia (Luka 2:10-14).

Hii ndiyo krismas ya kwanza, na kama unavyoona ilifanywa na Malaika. Mkazo wao ulikuwa nini? Je ni siku? la sivyo. mkazo wao ulikuwa: "habari njema ya furaha kuu wa watu wote." Hii habari njema ni kwamba amezaliwa kwa ajili ya kila mtu Mwokozi, Kristo Bwana, hii ina maana kuwa dunia imempata mmoja mwenye uweza wa kumwokoa kila mtu na dhambi zake, taabu zake, na kumpa kila aliyekata tamaa tumaini jipya la uzima wa milele. Hii ina maana kuwa kila mwenye dhambi sasa aweza kupokea uzima bure na kuifanya mbingu kuwa nyumbani kwake. Siku ile aliyozaliwa Bwana ilikuwa ni mapambazuko mapya, ilikuwa ni asubuhi mpya kwa dunia iliyokuwa imewekwa kwenye giza la uvuli wa mauti tangu alipoanguka Adamu baba yetu dhambini. Jua la haki lilizuka likiwa na uponyaji katika mbawa zake, Jua hilo ndiye Yesu, aliyefanyika kuwa jibu kwa kila nafsi iliyochoka, na isiyo na matumaini. Krismas inatuonesha neema kuu ya Mungu aliyetujilia tukiwa wafu kiroho, na waliohukumiwa kwenda jehanamu ya moto, na kutuletea wokovu huu mkuu kwa mkono wa Mwanawe Yesu Kristo.

Huu ndio ujumbe wa Krismas, na ndio tupaswao kuusisitiza, sio siku. Aha, hivyo basi kumbe kwa Mkristo wa kweli, Krismas ni kila siku, ila tu siku tuliyokubaliana kuitenga inatupa nafasi ya kuweka mkazo wa pamoja, na mazingira ya kuuambia ulimwengu uache kutukuza siku na badala yake uinue macho na kumtazama Yesu Kristo awaokoe, na kuwapa ushindi maishani kwani yeye ndiye amani yetu. Waliompokea Yesu wanapokusanyika pamoja mioyo yao huimba "atukuzwe Mungu juu mbinguni, na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia." Hao kama "kusanyiko la Kristo" ndiyo Krismas yenyewe, siyo siku. Ikumbukwe kuwa Krismas ni "Christ's Mass" yaani "kusanyiko la Kristo."

Hii ina maana kuwa kwa mkristo wa kweli Krismas ina mikazo miwili; wa kwanza ni mkazo wa kuelekea juu (vertical emphasis) na mkazo wa kuelekea kwa watu (horizontal emphasis). Mkazo wa juu ni wa ibada. Huu unadai kudumisha moyo wa ibada kwa Mungu na shukrani kwa neema yake aliyotupatia kwa kumleta Kristo kwetu. Malaika walitazama juu wakisema "atukuzwe Mungu juu mbinguni." Mkazo kwa watu unadai tuwapelekee wengine hizi "habari njema kwa watu wote" ili nao wapate wokovu wapokee "amani" ya mioyo yao na kufanyika sehemu ya "kusanyiko la Kristo" ambalo ndilo Krismas ya kweli.

Wengi siku hii ya leo, wanasherehekea Krismas kwa ulevi, uasherati, ugomvi, na wivi. Katika hao, wengi wametoka makanisani mwao, wamepokea mahubiri kwa makasisi, wachungaji, na mpadre ambao nao yumkini mkazo wa mahubiri yao ni siku ya kuzaliwa kwa Mwokozi kuwa ni leo badala ya ile maana ya kuja kwake. Ni wangapi walioenda kanisani leo wamezaliwa mara ya pili na kuokoka? Wengine hata hawaamini kuwa kuna kuokoka duniani, lakini wanadhani bado wanasherehekea Krismas. Hivi haya makusanyiko mengi ya wasemao hakuna kuokoka, kisha wanadai kusherehekea Krismas hawajiulizi kuwa wao ni Kusanyiko la nani? Au wamesahau kuwa Krismas ni "Kusanyiko la Kristo?"